TUMA HABARI YOYOTE ULIYONAYO KWENDA zimetokelezea@gmail.com AU Whatsapp No 0716790749

Jaji mkuu Othuman Chande akizungumza na waandishi wa habari hivi karibuni. Picha na Maktaba
 
Dar es Salaam. Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam imefungua milango kwa mawaziri na wabunge kufunguliwa mashtaka kutokana na kauli watakazozitoa bungeni ambazo ni kinyume cha Katiba na Sheria.
Mahakama Kuu ilitoa msimamo huo jana wakati ikitoa uamuzi wa pingamizi la awali katika kesi ya kikatiba iliyokuwa ikimkabili Waziri Mkuu Mizengo Pinda, lililowasilishwa na Jopo la Mawakili wa Serikali wakiongozwa na Naibu Mwanasheria Mkuu wa Serikali (DAG, George Masaju.
Kesi hiyo namba 24 ya mwaka 2013 ilifunguliwa na Kituo cha Msaada wa Kisheria na Haki za Binadamu (LHRC) kwa kushirikiana na Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), dhidi ya Pinda na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG), aliyeunganishwa kama mlalamikiwa wa pili.
LHRC na TLS walikuwa wakidai kuwa Pinda alivunja Katiba kutokana na kauli aliyoitoa bungeni, wakidai kuwa ni amri kwa vyombo vya utekelezaji wa sheria kuwapiga wananchi wakati wa vurugu.
 
Hivyo, walikuwa wakiiomba mahakama, pamoja na mambo mengine, itamke kuwa kauli hiyo ni kinyume cha Katiba na imwamuru Pinda aifute hadharani.
Hata hivyo, Pinda na AG waliokuwa wakitetewa na DAG Masaju akisaidiana na Mawakili wa Serikali Wakuu (PSA, Gabriel Malata, Alecia Mbuya na Sarah Mwipopo), waliweka pingamizi la awali dhidi ya kesi hiyo, wakitoa hoja tano za kuomba kesi hiyo itupiliwe mbali.
Miongoni mwa hoja hizo ni pamoja na kwamba kesi hiyo ni batili na iko mahakamani isivyo halali kwa kuwa inakiuka Katiba ya Jamhuri ya Muungano ya Mwaka 1977 na Sheria ya Mamlaka, Kinga na Haki za Wabunge, ya mwaka 1988.
Mawakili hao walidai kuwa Pinda analindwa na Katiba Ibara ya 100 (1) na (2), ambazo zinamkinga mbunge kushtakiwa au kufunguliwa shauri la madai mahakamani kwa jambo lolote alilolisema, au alilolitenda, au alililoliwasilisha bungeni kwa njia ya maombi, muswada au hoja.
Mahakama Kuu katika uamuzi wake jana ilikubaliana na baadhi ya hoja za mawakili wa utetezi (Serikali) na kuitupilia mbali kesi hiyo, lakini ikatamka kuwa wabunge na mawaziri wanaweza kushtakiwa kwa kauli au jambo walilolitamka bungeni, linalokiuka sheria na haki za binadamu.
Uamuzi huo ulisomwa na Kiongozi wa Jopo la Majaji wa Mahakama Kuu, lililokuwa likisikiliza kesi hiyo, Jaji Kiongozi Fakih Jundu kwa niaba ya majaji wenzake, Agustine Mwarija na Dk Fauz Twaib.
 
Hata hivyo, jopo la majaji lilikataa hoja za utetezi kuwa wabunge wana kinga isiyo na mipaka ya kutokushtakiwa kwa kauli au jambo lolote walilolitamka bungeni.
 
Chanzo Mwananchi

0 comments :

 
Top