TUMA HABARI YOYOTE ULIYONAYO KWENDA zimetokelezea@gmail.com AU Whatsapp No 0716790749

Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe
     
Baada ya Watanzania kuliona Bunge likiwachukulia hatua vigogo waliohusika na ufisadi wa Akaunti ya Tegeta Escrow wa Sh306 bilioni, madudu mengine ya Serikali yanatarajiwa kubainika mara bada ya Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuanza kufuatilia sakata ya sukari nchini.
Hatua hiyo ya PAC kuanza kulifanyia kazi inatokana na malalamiko ya wamiliki wa viwanda vya sukari yanayotolewa kutokana na soko la ndani kutekwa na sukari inayoingizwa kutoka nje ya nchi na wafanyabiashara wakubwa.

Wiki iliyopita, Bunge lilifikia maazimio ya kutaka mamlaka za uteuzi ziwachukulie hatua kwa mujibu wa sheria, Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospter Muhongo na katibu mkuu wa wizara hiyo, Eliakim Maswi, Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Profesa Anna Tibaijuka na Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Frederick Werema kutokana na kuhusika kwao kwenye sakata la uchotwaji wa fedha hizo kwenye akaunti ya escrow na kupokea fedha hizo.

Mwenyekiti wa PAC, Zitto Kabwe anasema malalamiko na matatizo yaliyopo, watatumia kipindi cha mwezi huu na ujao kupitia suala la sukari kwa kuwa ni kubwa kuliko hata ufisadi uliojitokeza katika akaunti hiyo ya Tegeta Escrow.

“Hili suala la sukari ni kubwa kuliko hata la escrow kwani linagusa moja kwa moja maisha ya wananchi, wamiliki wa viwanda na uzalishaji na tayari tumeiita Bodi ya Sukari tujadiliane kwa kina kuhusu suala hili,” anasema Zitto.

Wamiliki wa viwanda Mkurugenzi wa viwanda vya sukari vya Kagera na Mtibwa, Seif Seif anasema hasara ambayo taifa litapata kutokana na kufungwa kwa viwanda hivyo ni kubwa kuliko serikali inavyofikiria.

Anasema jambo hilo linatokana na sukari inayozalishwa nchini- kwenye viwanda vyote vinne vya Kilombero, TPC, Kagera na Mtibwa- kuwa ni tani 320,000 huku mahitaji yakiwa ni tani 420,000.

Seif anasema kutokana na upungufu wa tani 100,000, walikubaliana na Serikali kwamba iwe inaagiza tani 100,000 ili kufidia upungufu huo, jambo ambalo linafanywa kinyume na makubaliano yao.
 “Leo hii ukipita katika maduka mbalimbali, utakunata na sukari ya kila aina huku sukari yetu ikiwa imesheheni katika maghala tukiwa hatujui wapi pa kuipeleka...na hao wanaoingiza sukari hiyo ni ushirikiano na vigogo wa serikali, jambo ambalo kwa sasa limeota mizizi na hatua za makusudi hazionekani.
“Tatizo hili linajulikana kuanzia ngazi za juu kabisa za uongozi kwani sio geni na kutokana na hali hiyo sisi wamiliki hatuoni sababu ya kuendeleza viwanda hivyo kwa hasara. Ni bora tuvifunge na tuangalie majukumu mengine ya kufanya,” anasema Seif.
Kutokana na ugumu wa biashara, Seif anasema wamepunguza wafanyakazi 2,000 na kubakiwa na 5,000 kwenye Kiwanda cha Kagera, Kilombelo 3,000 na wamebaki 6,000 na Mtibwa 3,000 wakikosa kazi kutoka wafanyakazi 6,000.
“Fikiria watu hawa ambao walikuwa wanafanya kazi katika viwanda hivi, wanakwenda wapi? Lakini hawa nao waliobaki tukivifunga watakwenda wapi? Hili ni swali ambalo Serikali inatakiwa kujiuliza baada ya sisi kufunga viwanda itawasaidiaje wananchi hawa ambao najua kabisa kwamba wana familia na wanategemewa?” anasema Seif.
Anasema uwekezaji wa sukari unahitaji uvumilivu kwani ili uanze kupata faida ni zaidi ya miaka 10 ukiwa hujapata kitu kutokana na maandalizi yake kuchukua muda mrefu hivyo serikali inatakiwa kuhakikisha inavilinda viwanda vya ndani ambavyo licha ya kuwekeza pia inasaidia katika huduma za jamii.
Mwenyekiti wa Bodi ya Kiwanda cha Sukari Kilombero, Ami Mpungwe anasema: “Hali ni mbaya, tunaona kuliko kuendelea na hali hii ni bora tufunge kuzalisha sukari kuliko kuendelea.
“Kama kweli Serikali ina dhamira ya kuvifufua na kuviendeleza viwanda vyetu vya ndani, ni lazima kuvilinda na kupiga marufuku uagizwaji holela wa sukari kutoka nje.”
Mpugwe anasema kufungwa kwa viwanda hivyo kutaathiri hata wakulima wadogo kwani watakosa sehemu ya kuuza miwa yao kwa kukosa soko, jambo ambalo pia litarudisha nyuma maendeleo ya wakulima hao.

0 comments :

 
Top