Ndugu Wananchi;
Kama mjuavyo uhusiano wetu na Rwanda umekuwa mzuri kwa miaka mingi.
Tunashirikiana na kusaidiana kwa mambo mengi baina ya nchi zetu kitaifa
na katika kanda yetu ya Afrika Mashariki na Nchi za Maziwa Makuu, katika
Umoja wa Afrika na hata kimataifa. Uhusiano unaelekea kupata mtikisiko
baada ya mimi kutoa ushauri kwa Serikali ya Rwanda kuzungumza na
mahasimu wao. Ushauri ule niliutoa kwa nia njema kabisa kwani bado
naamini kuwa kama jambo linaweza kumalizwa kwa njia ya mazungumzo njia
hiyo ni vyema itumike. Isitoshe, ushauri ule niliutoa pia kwa Serikali
ya Kongo na kwa Serikali ya Uganda. Katika mkutano ule Rais Yoweri
Museveni wa Uganda aliunga mkono kauli yangu. Rais wa Rwanda hakusema
cho chote pale mkutanoni. Baada ya kurudi nyumbani ndipo tukaanza
kuyasikia maneno tuliyoyasikia na tunayoendelea kuyasikia.
Kwa kweli nimestaajabu sana na jinsi walivyouchukulia ushauri wangu na wanayoyafanya. Havifanani kabisa, completely out of proportion and out of context.
Mimi nilifanya vile kwa kuzingatia mila na desturi zetu za miaka mingi
katika ukanda wetu. Tumekuwa tunakutana katika mikutano na vikao
mbalimbali tunazungumza na kushauriana kwa uwazi juu ya njia za
kushughulikia matatizo na masuala mbalimbali kila yanapotokea. Wakati
wote tumeyachukulia kuwa ni mambo yanayotuhusu sote hivyo kupeana
ushauri ni wajibu wetu wote. Na mara nyingi ushauri kwa wanaogombana
kuzungumza tunautumia sana. Iweje leo mtu kutoa ushauri ule lionekane
jambo baya na la ajabu. Jambo la kushutumiwa na kutukanwa! Siyo sawa
hata kidogo!! Ushauri si shuruti, ushauri si amri. Una hiyari ya
kuukubali au kuukataa. Muungwana hujibu: “Siuafiki ushauri wako”.
Hakuna haja ya kutukana wala kusema maneno yasiyostahili wala kusema
yasiyokuwepo na ya uongo.
Ndugu Wananchi;
Napenda kurudia kusema kuwa mimi binafsi na Serikali yetu ya Tanzania
hatuna ugomvi wala nia yo yote mbaya na Rwanda. Tunapenda tuendelee
kuwa na uhusiano mzuri na Rwanda. Labda wenzetu wanalo lao jambo dhidi
yetu ambalo sisi hatulijui. Maana na sisi tunasikia mengi
yanayozungumzwa na kudaiwa kupangwa kufanywa na Rwanda dhidi yangu na
nchi yetu. Hatupendi kuyaamini moja kwa moja tunayoyasikia lakini
hatuyapuuzi.
Source: Hotuba ya Rais Mwisho wa Mwezi Julai 2013
Home
»
»Unlabelled
»
KIKWETE AMPA KAGAME VIDONGE VYAKE KATIKA HOTUBA YAKE
Subscribe to:
Post Comments
(
Atom
)
0 comments :
Post a Comment