Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), imetoa mwongozo ikisema kuwa matokeo ya
udiwani, ubunge na urais yanayobandikwa kwenye vituo mbalimbali nchini
ni ruksa kutangazwa na vyombo vya habari, lakini havina mamlaka ya
kumtangaza mshindi wa nafasi yoyote.
Kamishna wa Nec, Prof. Amon Chaligha, alitoa mwongozo huo wakati akijibu
maswali ya wahariri wa vyombo mbalimbali vya habari waliotaka kujua
kama vyombo vyao vitaruhusiwa kutangaza matokeo ya urais kadiri
yatakavyokuwa yakipokelewa kutoka kwenye vituo mbalimbali nchini.
Alisema awali, matokeo ya urais yalikuwa hayabandikwi wala mawakala
kusomewa, lakini sasa imeamuliwa yasomwe, yabandikwe na kila mmoja
kupewa nakala kwa lengo la kuongeza uwazi.
“Matokeo ya vituo yanaruhusiwa kujumlishwa na kutangazwa… waandishi wa
habari wanaweza kutangaza matokeo ya vituo, lakini siyo kutangaza
mshindi,” alisema Profesa Chaligha na kuongeza:
“Tunafanya hivi ili kuondoa hisia mbaya na kuziba mianya ya kuibwa kwa
kura au kubadilishwa matokeo. Tume haina matokeo yake kama inavyosemwa,
bali ni yale yatokanayo na kura zinazopigwa na wananchi,” alisema.
“Tangazeni matokeo, lakini msiandike huyu ni mshindi kwa sababu hiyo si kazi yetu,” alisema.
“Tangazeni matokeo, lakini msiandike huyu ni mshindi kwa sababu hiyo si kazi yetu,” alisema.
Kwa mujibu wa kifungu cha 80 cha sheria ya Tume ya Taifa ya Uchaguzi
sura ya 343 na kifungu cha 81 cha sheria ya uchaguzi ya serikali za
mitaa, sura ya 292, Nec ndiyo yenye mamlaka kisheria kujumlisha na
kutangaza matokeo ya uchaguzi wa rais.
Wasimamizi wa uchaguzi wa majimbo husika ndiyo wenye mamlaka kisheria
kujumlisha na kutangaza matokeo ya uchaguzi ya ubunge na wasimamizi
wasaidizi wa uchaguzi ndiyo wenye mamlaka ya kujumlisha na kutangaza
matokeo ya udiwani.
JAJI LUBUVA ATOA NENO
Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva, alivitaka vyombo vya habari kuzingatia maadili ya kazi yao kwa kuendelea kuandika ukweli bila kuegemea upande wowote.
Mwenyekiti wa Nec, Jaji Damian Lubuva, alivitaka vyombo vya habari kuzingatia maadili ya kazi yao kwa kuendelea kuandika ukweli bila kuegemea upande wowote.
“Tunaomba mtumie kalamu zenu kuelimisha wapigakura wajitokeze kushiriki uchaguzi mkuu,” alisema.
Kamishna wa Nec, Jaji mstaafu John Mkwawa, pia alifafanua juu ya
wapigakura ambao walirekebisha taarifa zao, lakini hadi siku ya uchaguzi
majina yakakosekana katika Daftari la Kudumu la Wapigakura, akisema
kuwa kitakachotumika kuwaruhusu kupiga kura ni hekima na burasa ya
msimamizi wa kituo baada ya kujiridhisha na kitambulisho
kitakachoonyeshwa na mpigakura.
Mkurugenzi wa Nec, Ramadhani Kailima, alisema hadi kufikia Oktoba 15,
vifaa vyote vya uchaguzi vitakuwa vimeshawasili katika majimbo yote
nchini isipokuwa karatasi za kupigia kura ambazo alisema zitawasili
baadaye.
Chanzo: NIPASHE
0 comments :
Post a Comment