TUMA HABARI YOYOTE ULIYONAYO KWENDA zimetokelezea@gmail.com AU Whatsapp No 0716790749



Kwa upande wa viongozi wa kisiasa ambao waliingiziwa fedha katika akaunti zao binafsi ni; Mhe. Andrew Chenge (Mb), ambaye alikuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali na sasa ni Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti, shilingi bilioni 1.6; Mhe. Anna Tibaijuka (Mb) na Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi shilingi bilioni 1.6; Mhe. William Ngeleja (Mb) na ambaye alikuwa Waziri wa Nishati na Madini shilingi milioni 40.4 na Ndg. Daniel N. Yona ambaye alikuwa pia Waziri wa Nishati na Madini shilingi milioni 40.4; Ndg. Paul Kimiti ambaye ni Mbunge Mstaafu wa Jimbo la Sumbawanga shilingi milioni 40.4 na Dr. Enos S. Bukuku ambaye alikuwa Mjumbe wa Bodi ya TANESCO aliingiziwa shilingi milioni 161.7.

Upande wa Viongozi wa Madhehebu ya Dini walioingiziwa fedha na Benki ya Mkombozi ni Askofu Methodius Kilaini shilingi 80.9, Askofu Eusebius Nzigirwa shilingi milioni 40.4 na Mchungaji Alphonce Twimann Ye Simon shilingi milioni 40.4

Kamati ilithibitishiwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU kuwa baadhi ya watu walienda kugawana fedha kwenye Benki tajwa wakiwa na mifuko ya rambo, sandarusi, mabox, magunia na lumbesa. Kutokana na muamala uliofanyika tarehe 6 Februari, 2014 katika Benki ya Mkombozi kiasi cha shilingi bilioni 3.3 na muamala wa Benki ya Stanbic wa tarehe 23 Januari 2014 ambapo fedha taslimu (cash) kiasi cha shilingi bilioni 73.5 zilitolewa na kugawanywa kwa watu mbalimbali kinyume cha Sheria ya Benki Kuu na Taasisi za Fedha ya mwaka 2006

Aidha Taasisi ya Kuzuia na kupambana na Rushwa (TAKUKURU) na Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai (DCI) mara moja wachukue hatua ya kumkamata Bwana Harbinder Singh Sethi na kumfikisha mahakamani kwa makosa ya Anti money laundering , ukwepaji kodi na wizi. Kamati pia inaelekeza Serikali kutumia sheria za Nchi, ikiwemo sheria ya ‘ Proceeds of Crime Act ’ kuhakikisha kuwa Bwana Harbinder Singh Sethi anarejesha fedha zote alizochota kutoka Benki Kuu ya Tanzania. Kwa kuwa suala hili ni suala la utakatishaji wa fedha haramu, Mamlaka ziwasiliane na mamlaka za Nchi nyingine kuhakikisha mali za Bwana huyu zinakamatwa na kufidia fedha hizo.

Kwa mujibu wa Taarifa ya CAG na kuthibitishwa na Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU fedha hizo pia ziligawiwa kwa watu mbalimbali binafsi. Kamati haina tatizo na watu wawili kuuziana makampuni yao kwa thamani wajuazo wenyewe, au jinsi ya kuzitumia fedha zao, ama kuwachagulia watu wa kuwagawia, lakini Kamati imejidhihirishia kuwa fedha iliyotumika kulipia manunuzi hayo ni fedha ambayo sehemu yake ni ya umma iliyochotwa bila huruma wala aibu, kutoka Benki Kuu. Hivyo, Kamati inazitaka mamlaka za uchunguzi kuhakikisha kuwa fedha hizo zinarudi Benki Kuu hata ikibidi kwa kufilisi mali za watu wote 97 waliofaidika na fedha hizo kwa thamani ya fedha walizopewa na Bwana Rugemalira

Baadhi ya waliofaidika na fedha hizo ni Viongozi wa Umma ambao wanapaswa kuzingatia Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma (Sheria namba 13 ya Mwaka 1995) ambayo inawataka kutoa taarifa ya zawadi wanazopokea au malipo wanayolipwa. Vyombo vya uchunguzi vifanye uchunguzi kutambua kama walifuata matakwa ya sheria na hatua mahsusi zichukuliwe, ikiwemo kuvuliwa nyadhifa zao zote za kuchaguliwa na/au kuteuliwa, kufilisiwa mali zao na kushtakiwa mahakamani kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, ibara ya 132 (1) – (6). 

Kamati imejiridhisha kwamba, suala la akaunti ya Escrow ni jambo la utakatishaji wa fedha (Money Laundering), kama alivyosema Mkurugenzi Mkuu wa TAKUKURU katika mahojiano yake na Kamati. Kamati inazitaka mamlaka zinazohusika, ikiwemo Benki Kuu kuzitangaza benki za Stanbic na Mkombozi Commercial Bank kama asasi za utakatishaji fedha (Institutions of Money Laundering Concern).

Aidha, Kamati inalikumbusha Bunge lako tukufu pendekezo muhimu lililotolewa na Kamati Teule ya Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe kuhusu sakata la maarufu la Richmond

Kamati inapendekeza kwamba, azimio hili litekelezwe kwa kupitia upya mikataba yote ya umeme ambayo inalitafuna Taifa letu.

Aidha, Kamati imebaini kuwa Waziri wa Nishati na Madini ndiye alikuwa dalali mkuu aliyewakutanisha Bwana Harbinder Singh Sethi na Bwana James Rugemalira, tena katika ofisi ya Umma; na pengine hii ndiyo iliyokuwa sababu ya upotoshaji huu. Waziri wa Nishati na Madini alifanya udalali huo akijua dhahiri kuwa Bwana Sethi hana uhalali wa kisheria kufanya biashara kwa jina la IPTL. Iwapo Waziri wa Nishati na Madini angetimiza wajibu wake ipasavyo, Fedha za Tegeta ESCROW zisingelipwa kwa watu wasiohusika, na Nchi ingeweza kuokoa mabilioni yaliyopotea kama kodi za VAT, Capital Gain Tax na Ushuru wa Stempu ambazo ni sawa na takribani shilingi bilioni 30.

Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kuwa Mamlaka yake ya uteuzi itengue uteuzi wa Waziri wa Nishati na Madini kutokana sababu hizo zilizoelezwa.

Kamati pia imethibitisha uzembe wa hali ya juu uliofanywa na Katibu Mkuu huyo, kushindwa kujiridhisha kama masharti ya Sheria ya kodi ya Mapato Sura ya 333, Kifungu cha 90(2) yalitekelezwa. Kifungu hicho kimsingi kinaitaka mamlaka ya ‘ approval ’’ ya uhamishaji wa Makampuni kutotambua Kampuni mpaka kwanza kodi za uhamishaji ziwe zimelipwa na hati za malipo ya kodi zimetolewa na mamlaka ya kodi. Mheshimiwa Spika, Kamati inapendekeza kuwa uteuzi wa Katibu Mkuu huyu utenguliwe, na TAKUKURU wamfikishe mahakamani mara moja, kwa kuikosesha Serikali Mapato, matumizi mabaya ya ofisi na kusaidia utakatishaji wa fedha haramu.

Kamati imethibitisha kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali alitoa ushauri ulioipotosha Benki Kuu ya Tanzania kuhusiana na hukumu ya Jaji Utamwa J. Kwa kutumia madaraka yake vibaya, Mwanasheria Mkuu wa Serikali aliagiza kodi ya Serikali yenye thamani ya shilingi 21 bilioni isilipwe 106 na hivyo kuikosesha Serikali mapato adhimu. Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa kujua na kwa makusudi alilipotosha Bunge na Taifa kwamba mgogoro uliopelekea kufunguliwa kwa Akaunti ya ESCROW ulikuwa ni mgogoro wa Wanahisa wa IPTL badala ya mgogoro kati ya TANESCO na IPTL. Kamati inapendekeza kuwa uteuzi wa Mwanasheria Mkuu wa Serikali utenguliwe mara moja na kisha afikishwe mahakamani kwa matumizi mabaya ya Ofisi yaliyopelekea Serikali kupoteza mabilioni ya fedha. 

Baada ya kupitia vielelezo vilivyomo kwenye ripoti ya CAG, Kamati imejiridhisha pasipo mashaka kuwa, Waziri Mkuu, alikuwa ana taarifa zote kuhusiana na mchakato mzima wa kuchotwa fedha kutoka katika akaunti ya ESCROW.

Kamati, kwa kuzingatia kielelezo namba 22, inathibitisha bila shaka kwamba, Waziri Mkuu alikuwa analijua jambo hili vizuri na kwamba aliridhia muamala huu ufanyike. Ndiyo maana katika maelezo yake ya Bungeni mara kadhaa Waziri Mkuu alithibitisha kuwa fedha za Escrow hazikuwa fedha za Umma.

Ni dhahiri kwamba viongozi wenye mamlaka makubwa wanapaswa kila wakati kukumbuka kauli ya muasisi wa Mapinduzi ya Zanzibar na Muasisi wa Muungano, Sheikh Thabit Kombo, ambaye alikuwa akipenda kusema ‘ weka akiba ya maneno.

Kwa uzito na unyeti wa jambo hili, kwa vyovyote vile, Waziri Mkuu anapaswa kuwajibika kwa kauli zake na kwa kutokutekeleza wajibu wake wa kikatiba ipasavyo, ili kurejesha imani ya wananchi kwa serikali yao na viongozi wao wa kisiasa.


0 comments :

 
Top