TUMA HABARI YOYOTE ULIYONAYO KWENDA zimetokelezea@gmail.com AU Whatsapp No 0716790749




Na Khelef Nassor
Zanzibar: Mgombea wa urais wa Zanzibar kupitia Chama cha Wananchi CUF anayeungwa mkono na vyama vinavyounda Ukawa, Maalim Seif Sharif Hamad amesema akichaguliwa kuwa rais, ataifanya Bandari ya Zanzibar kuwa huru ili wananchi waweze kuingiza bidhaa zao bure nchini.
“Mkinichagua, nitaifanya bandari ya Zanzibar kuwa huru ili kutoa fursa kwa vijana wetu kupata ajira. Sisi tunataka kila kijana mwenye uwezo wa kufanya kazi apate ajira” Alisema.
Katika hotuba yake aliyoitoa hapo jana mbele ya wananchi wa Jimbo la Mfenesini ambao walikusanyika kwa wingi katika uwanja wa Mwakaje, Maalim Seif aliahidi kutatua kero za wakulima na wafugaji kwa kuwajengea mazingira wezeshi ambayo yatawasaidia kupata soko la uhakika.
“Tutatilia mkazo kwenye kilimo na ufugaji wa kisasa ili viweze kuleta tija kwa wakulima, Tutaimarisha sekta ya ufugaji kwa kutilia mkazo ufugaji wa n`gombe wa kisasa ambao watatoa maziwa mengi kwa kuingiza mbegu bora” Alisema Maalim Seif huku akishangiriwa na maelfu ya wananchi waliokusanyika uwanjani hapo.
Akizungumzia suala la Elimu, Maalim Seif ambaye pia ni Makamo wa Kwanza wa rais wa Zanzibar, amesema ataiboresha sekta hiyo na kuahidi kuwa elimu itakuwa bure kwa ngazi zote ili kutoa fursa wananchi wenye hali duni kuweza kujipatia elimu.
“Tutaijenga elimu kwa kuifanyia marekebisho makubwa ili iweze kufikia kiwango cha kimataifa” Alisema.
Hata hivyo amesema ameandaa mipango madhubuti ya kuboresha sekta ya afya ambayo imekuwa nyuma kwa takriban miaka 50 katika kuwahudumia wananchi na hivyo ameahidi kuiga mfumo kutoka nchi nyengine katika uboreshaji wa sekta hiyo.
“Tutatumia mfumo wa Oman wa Kuangalia tangu kidonge kinapoingia hadi kumfikia mgonjwa ili tuhakikishe kidonge hicho kinamfikia mlengwa” Alisema Maalim Seif na Kushangiriwa na wananchi.
Mgombea huyo ambaye amekuwa akipiga vita suala zima la ubaguzi alisema: “Wako viongozi wa CCM wanaowadanganya wananchi kuwa eti kuwa nikipata urais nitawafukuza vijana kutoka bara, hilo si kweli!, katika uongozi wangu nitahakikisha watu wote wanakuwa sawa, na hata vijana kutoka bara watapata haki sawa na Wazanzibari”.
Maalim Seif ambaye aliambatana na Kampeni meneja wake Nassor Mazrui, mara baada ya kumaliza hotuba yake, aliwataka wananchi kumchagua na kumuunga mkono Mgombea wa urais wa Jamhuri ya Muungano kupitia Chadema na Ukawa, Edward Lowassa kwani ndiye kiongozi pekee atakayeweza kuleta maendeleo kwa Watanzania.

0 comments :

 
Top