| Kocha wa Taifa Stars , Boniface Mkwasa akizungumzia mwenendo wa timu hiyo |
Dar es Salaam. Kocha Mkuu wa Taifa Stars, Charles Boniface Mkwasa amesema kikosi chake kilikuwa na tatizo ufundi na kukosa mazoezi ya ukakamavu, upungufu uliosababisha kufanya vibaya chini ya mtangulizi wake, Mart Nooij.
Mkwasasa aliyeiongoza Stars kutoka sare ya goli
1-1 dhidi ya Uganda Cranes Jumamosi iliyopita aliwaambia wanahabari jana
kuwa kabla ya mechi hiyo, asilimia kubwa ya wachezaji wa Stars walikuwa
na kasoro kubwa mbili.
“Tanzania hatukustahili kufungwa na Uganda, kama
tungeitumia mechi yetu ya nyumbani vizuri, matokeo ya ugenini ya 1-1
yangetubeba, lakini kuna kitu ambacho nadhani kocha aliyepita
hakuzingatia.
“Wakati nakabidhiwa timu nilichokigundua ni
kwamba, wachezaji wengi hawakuwa na utimamu wa mwili na ufundi, hizo
zilikuwa kasoro kubwa kwa timu yetu, nilijaribu kuwa nao kwa kipindi
kifupi nilichokabidhiwa na taratibu wameanza kubadilika,” alisema.
Akizungumzia mchezo na Uganda Cranes, Mkwasa
alisema, “Vijana wangu walicheza vizuri hata wenyeji hawakutarajia, kila
mmoja alishangaa ni vipi walitufunga nyumbani mabao 3-0, ilifikia
mahali baada ya kuzidiwa walitumia mbinu zisizofaa ili kututoa mchezoni.
“Kama tutaendelea hivi na kuungwa mkono, hakuna ubishi Stars itafika mbali,” alisema.
Aidha, Mkwasa alieleza kuwa, baada ya michuano ya
Kombe la Kagame, Stars itaingia kambini kujiweka fiti kwa ajili ya
mchezo wao wa Septemba 4 dhidi ya Nigeria wa kufuzu kushiriki fainali za
mataifa ya Afrika (Afcon) 2017.
0 comments :
Post a Comment