TUMA HABARI YOYOTE ULIYONAYO KWENDA zimetokelezea@gmail.com AU Whatsapp No 0716790749

“Human is Politically Animal” ni mwanafalsafa wa Kigiriki Aristotle aliyanena haya miaka mingi kabla ya ujio wa Yesu Kristo .Unajua alimaanisha nini? Huwezi kuikwepa siasa kwenye maisha ya kila siku,na nilizidi kukubaliana na hili miezi kadhaa zilizopita nikiwa na rafiki yangu ninayesoma naye tukiwa kituo cha daladala Mwananchi,Tabata tukisubiri daladala kuelekea katika ofisi za gazeti la Nipashe nilizofika kwa mara ya kwanza siku hiyo.
Watanzania ni wazungumzaji wazuri, kuingia tu ndani ya daladala,mazungumzo yaliyotawala kwa asilimia kubwa ni juu ya siasa za  “kibongo”. Kutokana msongamano nilitamani nifike karibu na siti mbili za mwisho “soga” liliponoga hata niwasikilize kwa umakini.
Jamaa mmoja wa makamo alidai   “Watanzania “wanajitambua” tayari huwezi kuwadanganya kwasasa”. Walio wengi wakaenda mbali kwa kupinga wakidai hali ya nchi ilipofikia inatia shaka kiuchumi haswa kutokana na utekelezaji mbovu wamikakati ,hao wananchi wenye utambuzi wamechukua hatua gani kama demokrasia ipo mikononi mwao?
Kwangu mimi na fikra zangu nikasema Watanzania wapo katika  “mchakato” wa kujitambua kwa kuwakumbukusha  asilimia 80 ya kura za uchaguzi wa 2005 na asilimia 61.7  za 2010 alizoshinda Mheshimiwa Rais Jakaya Kikwete,basi Watanzania wanazidi kupata elimu juu ya masuala yao ya kimsingi  siku zinavyozidi kwenda,umaarufu wa CCM unapungua kama wao ni kikwazo.
Hili suala la ufisadi na hakuna ajira,wananchi wamechoka na  mtazamo wa baadhi yao wakadai bora itokee “VITA”.Hapo ndipo nikachangia nikasema tusifike kwenye “SIASA NYEKUNDU” yaani kumwaga damu(ikiwemo vita), kwenye “SIASA NYEUSI”  iliyopo sasa ya kudanganywa na ufisadi uliokithiri tuitengeneze kuwa “SIASA NYEUPE” kwa kura za haki kwa wingi tumweke kiongozi mwajibikaji. Jamaa mmoja wa makamo akaniambia “acha kuwa mwoga”,   ikabidi ninyamaze kidogo wakiendeleza “ ugomvi wa maneno”.Baadhi yao wakisema bora vita katika kudai haki, iweje Waarabu wamezoea?
Jamani vita inazoeleka kweli waungwana ?Nikagundua kuna watu  wanaopenda kubishana tu pasipo kuwa na “mpangilio mzuri wa fikra”  ili safari ndefu ya daladala na foleni iishe. Nikakumbuka kumbe nipo jiji la Dar es Salaam. Sikuwalaumu.
Sikupenda kuendelea kubishana nao, kuna ndugu mmoja wa makamo nikamwita “anko” nikamwambia hali tutaibadilishaje wakati viongozi wamewahadaa wananchi maisha bora na ajira kwa vijana imebaki kitendawili na mteguaji hajulikani na ndio sababu baadhi ya Wananchi wanasema watumie njia nyingine kimtazamo wa kawaida zisizo na mfanano na mazingira ya kitanzania. Fikra zikamkumbuka shujaa aliyeuwawa kwa kutetea haki za Watu weusi Marekani Malcom X  alisema “If you’re not ready die for it put the word freedom out of your mouth”- kwa tafsiri isiyo rasmi ni kuwa “ kama huwezi kuifia, ondoa neno uhuru mdomoni mwako” lakini alikuwa sahihi. Inawezekana  kwa mapambano yale ni wazi kujitoa kwa namna ile kulihitajika, muda unakwenda zama zinabadilika. Siku hazigandi, mabadiliko. Kupiga kura hasa vijana kwa chaguzi zlizopita imekuwa ya kusuasua. Je hatua wanayowaza inakuwaje? Ukomavu wa kisiasa wa hivyo hatujafikia.
 Watanzania cha kufanya ni kuigeuza kuwa “SIASA NYEUPE” yaani siasa safi na  kura kwa sasa ndio silaha,haya tujiandikishe kwa wingi tumweke mwajibikaji na mzalendo.Nikakumbushia lile balaa la Arusha la milipuko ya mabomu, eneo la Sanawari na Maeneo baadhi  Arusha mjini, watu hawakukaa kwenye maeneo yao ya biashara ,kila kona mbio,vipi mabomu ya machozi yanavyozima  migomo ya wanachuo? Hilo la “SIASA NYEKUNDU” hatujalifikia hilo, dawa ni KUANDAA KURA YAKO VYEMA.
Yaliyotokea Tanzania Visiwani baada ya uchaguzi, mwaka 2001 ya wafuasi wa CCM na CUF kushambuliana, sipendi kuyasikia  tena!
Unadhani Baba wa Taifa alikuwa “mjinga” kusita kuingia kwenye vita kirahisi na kuamua kufanya maamuzi magumu kuruhusu Jeshi letu kakamavu likapambane? Unajua alichofanya nasikia alikesha na rozari kanisani usiku kucha?Alikuwa muumini mzuri wa “imani” Alijua madhara yake,Uchumi ulikuwaje baada ya vita? Wazee wetu wanayo majibu.Uchumi ulishuka sana.
Yule niliyemwita “anko” alinikumbusha habari niliyohadithiwa na mjomba wangu aliyesoma na kina Mheshimiwa Rais Kikwete pale Shule ya Tanga (Tanga School ) enzi za  Mwalimu Mkuu wa fikra yakini J.K Nyerere, juu ya Elimu, Chakula(asubuhi chai nzito), na usafiri wa  bure kwa gharama za Serikali. Akaniuliza leo hii nyie madaftari ni elfu moja mpaka elfu tatu, fedha  ya kitanzania, halafu tuna misitu mikubwa nchini?
Nikawaza hali ya shule za msingi hakuna madawati ,Vyuo Vikuu kuna suala mikopo,watoto wa wakulima tunavyojikaza, nani atakufikiria .
Nikazama kifkra zaidi nikakumbuka miezi  ya karibuni, Mheshiwa Joseph Mbilinyi “Sugu”  yule nguli wa mziki wa kufoka foka ( Hip Hop), mbunge wa Mbeya Mjini pale kwenye Bunge la Katiba alichokisema juu ya Serikali isivyosikivu juu ya ushauri wa Vyama pinzani kuhusiana na Uboreshaji wa Daftari la Wapiga Kura unahitaji muda katika kuuandaa  na maswala mengine yenye maslahi kitaifa yasiyohitaji mgawanyiko wa itikadi na uchama  kwa kile alichosema nambari haidanganyi kwa kufanya mambo kwa  “ tathmini onyeshi” moja ni moja na nane si saba, nikagundua kuwa watu wana uzoefu na matukio haya kinyama kwa kuona kwenye “video” , kuhadithiwa  vita ya Kagera pasipo kushuhudia, na kusikia mauaji ya kimbari kule Rwanda kuwa yalipoteza maisha ya Watu kadhaa bila kutafakari kwa kina matokeo ya vitu wanavyofikiria.Wale wakimbizi pale Bulombora,Kigoma hali  ilikuwa inatishaje? Njaa, ambaye ni adui namba moja alihusika pale.
“Nyuma ya pazia” eti Israeli alipompiga Libya enzi za Kanali Muammar Qaddafi  miaka ya nyuma  katika sekeseke la Umoja wan nchi za Kiarabu (Arab League) alichokumbuka alimletea chakula cha msaada.Unajua waliwaza nini? Njaa kwa kuwa vita inaendelea nani anazilisha? tusiyawaze hayo Watanzania tukomae kuleta “Siasa Nyeupe”, na tunailetaje? Hili ndio suala la msingi na sio kusema wanatudanganya, na mfumo wao umekomaa. Utabadili sio maneno, mpiga kura akijua kilo za sukari kutoka kwa mgombea zilivyo kitulizo cha  njaa ya usiku kuamka  asubuhi kuna siku ndefu  tunaiita baada ya uchaguzi, ANDAA KURA YAKO.


Nikawaza mbali kwa kina  kuwakumbuka makada wa CCM  na mbio za kugombea  urais kupitia chama hicho, zaidi ya 30 walikuepo katika vikumbo vya kuingia kwenye “hekalu la kaisari” hatimaye Ndugu Dkt. John Magufuli akaibuka kidedea, chama kimepoteza sifa fulani, wanataka kuirudisha.Usishangae walivyotupiana madongo. Wanajua wanachofanya. ANDAA KURA YAKO VYEMA.
Nikatafakari nikajua kuna jambo walilifanya, yawezekana kuwaachia uhuru wananchi kutathmini nani anastahili na kuwatengeneza vijana waliotangaza nia njia na “CV” kwa miaka ijayo. ANDAA KURA YAKO SASA.
UKAWA wanasoma alama za nyakati ulidhani Ndugu Edward Lowassa wangemkataa kuwepo kwenye umoja wao, na hao wengine kama Ndugu Fredrick Sumaye! wamechanganya maarifa, hivyo akili hazijaganda, wanaelewa nini Wananchi wanahitaji. ANDAA KURA YAKO.
Ujasiri ni pale unapojua "SIASA" si tatizo bali tatizo ni picha na taswira iliyojengeka mtu kuwa "MWANASIASA" ndani ya jamii na jibu unalo ili kugeuza neno "politics is dirty game" kwa "KUPIGA KURA PEKEE WASHIKAJI!. 
Ukijiamini unafanikiwa, unaonekana shujaa kutoka kwenye dimbwi la mfumo usio na kweli kiutawala utaitwa msaliti ni bora kuliko kuonekana mnyenyekevu kwao halafu kwenye jamii uonekane kamuzu Banda wa Malawi. wazee wetu  ukiwauliza watakujibu enzi za kupigania uhuru walimwita  Dkt. Kamuzu Banda "aliyeolewa na mzungu" aliwabania waafrika haki zao , ndiyo nyimbo iliyokuwa kwenye mchamchaka.
Kwanini nimesema hayo?  Nakumbusha raia wote wasaliti kwa machinga, boda boda, mama ntilie , wasakatonge , wasio na ajira kwa kubali kununuliwa kwa kofia, khanga ,kilo za sukari ni bora uonekane umemsaliti rafiki yako anayetafuta uongozi kwa njia ya kuzunguka kuliko kuitwa "umeolewa nao" na jamii ni mbaya sana, laana mbaya kabisa! ANDAA KURA VYEMA!
Nikamwona kifkra shujaa wa India, Mahatma Ghandi na falsafa yake kuwa “I love your Christ but not your Christianity” nikimaanisha CCM na UKAWA ni sehemu salama na sera zenye weledi lakini  walioko ndani yake ndiyo kuna kila aina ya ubaya,udhalimu, na siasa chafu japo kuna wasafi na wenye kweli daima. Naipenda sera weledi yenye utekelezaji, itikadi ninayo,na “imani” kwa  mgombea yoyote mwenye misingi fanikishi ya kuileta “TANZANIA NINAYOITAKA”,mpya isiyo  ya “ skendo ya ESCROW, mauaji ya Mwandishi Mwangosi, kutekwa kwa Mwandishi Kibanda na Dkt. Ulimboka na kauli za kibabe za  “makaisari” wetu na sio  ushabiki wa chama. Haya yakifanikiwa mbona “SIASA NYEUPE” itaonekana kama UKIANDAA KURA YAKO VYEMA!
Watanzania ni wepesi wa kusahau kama 2015 zao la kura  litaleta watu makini, wazalendo,wenye dira elekevu, na misimamo binafsi   tutakuwa tumefikia kiwango kikubwa katika “mchakato” wa kujitambua na kuutambua ukweli na ule mtazamo wa siasa ni mchezo mchafu (politics is the dirty game) utaanza kufifia kama UKIANDAA KURA YAKO VYEMA!
Kura ni haki ya kila Mtanzania mwenye umri wa miaka 18 na zaidi, mwenye akili timamu na sababu  zingine muhimu,vijana ndio chachu ya mageuzi na sio kulalamika ni mchezo mchafu,tukajiandikishe, oktoba 25, mapema tujitokeze, kwani kura ya Mtanzania mmoja  mwenye “imani” na maneno ya Mwalimu Nyerere “ sababu tunayo,nia tunayo,uwezo tunao na nguvu tunazo”  ni muhimu kuliko kura za vichwa kumi zilizopewa   kilo mbilimbili za sukari na mgombea yule mwenye tai kubwa na maneno mengi  yenye asali shubiri.
Najinukuu mwenyewe tena kama nilivyoandika hapo juu, "nakumbusha tu raia wote wasaliti kwa machinga, boda boda, mama ntilie , wasakatonge , wasio na ajira kwa kubali kununuliwa kwa kofia, khanga ,kilo za sukari ni bora uonekane umemsaliti rafiki yako anayetafuta uongozi kwa njia ya yake  kuzunguka kuliko kuitwa "umeolewa nao" na jamii ni mbaya sana, laana mbaya kabisa inaweza tafuna mpaka viunoni mwako!

  PETER C. MMBAGA.

MWANAFUNZI CHUO KIKUU, TANZANIA


0 comments :

 
Top