TUMA HABARI YOYOTE ULIYONAYO KWENDA zimetokelezea@gmail.com AU Whatsapp No 0716790749


Na Khelef Nassor

Zanzibar: Chama cha wananchi CUF kimewataka wanachama na wapenzi wa chama hicho kuwa watulivu na wavumilivu katika kipindi hichi, kufuatia hatua ya kujiuzulu kwa Mwenyekiti wake wa chama Profesa Ibraahim Lipumba. Wito huo umetolewa na Kaimu Mkurugenzi wa Habari, Uenezi na Mawasiliano na Umma wa chama hicho mhesimiwa Ismail Jussa Ladhu wakati alipokuwa akizungumza na waandishi wa habari katika ofisi ndogo ya chama hicho huko Vuga mjini Unguja.
Akizungumzia hatua ya kujiuzulu kwa Mwenyekiti huyo, mheshimiwa Jussa amesema chama chama cha wananchi CUF kimezipokea taarifa hizo na wanaheshimu maamuzi yake kwani ni haki yake kikatiba na kidemkrasia.
Aidha emesema, Profesa Lipumba amekuwa na mchango mkubwa katika miaka yote 16 ya uwenyekiti wake kwa chama cha CUF, nafasi ambayo imemfanya awe kiongozi wao mkuu
“Kwa nafasi yake hiyo, pia ametoa  mchango mkubwa katika ujenzi wa demokrasia katika nchi yetu. Tunaithamini kazi hiyo na tutaendelea kumheshimu kwa utumishi wake mkubwa kwa chama chetu na nchi yetu. Tuamtakia kila la kheri katika mipango yake ya baadae” Jussa alisema.
Jussa ameendelea kusema kuwa, Chama Cha Wananchi CUF ni taasisi na kinaendeshwa kitaasisi, hivyo basi maamuzi yake yote yamekuwa yakifanywa kitaasisi kwa mujibu wa katiba na kanuni za chama.
Kwa upande wa historia ya chama cha CUF, Jussa amesema chama hicho kimepita katika dhoruba na misukosuko mingi lakini mara zote wamekuwa wakionesha uwezo mkubwa wa kuhimili dhoruba na misukosuko hiyo, na kusisitiza kuwa hawana hata chembe ya wasiwasi kwani mtihani huo watauvuka na kuwa chama imara zaidi.
Aidha ameeleza kuwa Chama cha wananchi CUF kimepanga kuitisha vikao vya dharura vya Kamati ya Utendaji ya Taifa na Baraza kuu la Uongozi la Taifa siku ya Jumapili, tarehe 9 Agosti, 2015 ili kujadili hatua hiyo na kufanya maamuzi juu ya hatua muafaka zinazopaswa kuchukuliwa katika kipindi hiki hadi hapo chama kitakapomchagua mwanachama mwengine kujaza nafasi hiyo ya Mwenyekiti.
Akizungumzia ushirikiano wa chama cha CUF na UKAWA, mheshimiwa Jussa amesema chama cha CUF kitaendelea na shughuli zake kama chama na pia kama mshirika wa UKAWA ambayo CUF ilikuwa ni katika waasisi wake. Hivyo amewahakikishia wanachama na watanzania wote kwa ujumla kwamba chama cha CUF kitatumia nguvu, uwezo, juhudi na maarifa yake yote kuhakikisha kwamba inaulinda UKAWA ambao unaonekana kuwa ni mwiba kwa CCM.
Profesa Lipumba amejiuzulu wadhifa wa uwenyekiti wa Chama Cha Wananchi CUF kufuatia kile alichoeleza kuwa ni kutokana na dhamira na nafasi yake kumsuta kwa kuwa katika umoja wao wa katiba ya wananchi UKAWA wameshindwa kuzingatia tunu za taifa ambazo ni pamoja na utu, uzalendo, uadilifu, umoja, uwazi na uwajibikaji.

0 comments :

 
Top