Vyombo vya
habari ni moja ya nyenzo muhimu katika jamii si tu! Katika kuhabarisha na
kuburudisha bali hata katika kuielimisha jamii yenyewe. Vyombo vya habari ni
muhimili wa nne wa taifa badala ya ile mitatu ambayo ni baraza la utendaji
linaloongozwa na raisi, mahakama na bunge.
Kumekuwa na
tabia kwa baadhi ya vyama vya siasa na wanasisa kuvitumia vibaya vyombo vya
habari wakati uchaguzi mkuu unapokaribia. Wanafanya hivyo ili kutimiza azma yao
ya kuingia madarakani. Kwa mfano vyombo vya habari hutumika kueneza propaganda
za wagombea wa chama kimoja zaidi na kuwachafua wa chama chengine. Kwa mfano
TBC na ZBC ambavyo vyote vinamilikiwa na serikali, hujikita zaidi katika kutoa
taarifa za chama tawala (CCM) zaidi kuliko vyama vyengine vya upinzani. Hii si
haki na ni ukiukwaji mkubwa wa demokrasia.
Kwa bahati
mbaya sana baadhi ya vyombo hivyo hudiriki kuyatekeleza hayo si kwa matakwa yao
binafsi bali ni kutokana na ushawishi mkubwa unaotoka upande wa wagombea na
chama husika. Mara nyingi ushawishi huo unatokana na fedha ambazo vyombo vya
habari hupokea kutoka kwa wanasiasa wanaosaka madaraka kwa udi na uvumba kiasi
cha kupelekea vyombo hivyo kukiuka maadili yake.
Kuna wakati
vyombo vya habari hudiriki hata kuyaficha maovu yaliyofanywa na chama Fulani
iwe ni CCM, CUF au CHADEMA, kwa kuyafunika maovu hayo kwa guo la uzuri na wema
(Propaganda). Kufanya hivyo ni kuwayumbisha wananchi na ukiukwaji mkubwa wa
misingi ya kimaadili kwa vyombo hivyo.
Kazi kubwa
ya vyombo vya habari kuelekea uchaguzi mkuu ni kutoa elimu kwa wapiga kura
ambayo itapelekea wao kufanya maamuzi sahihi juu ya mustakbali wa taifa lao
kwenye uchaguzi mkuu kupitia sanduku la kura. Inafaa tukumbuke kuwa asilimia
kubwa ya wapiga kura hawana elimu ya kutosha juu masuala ya uchaguzi, hivyo
basi ni wajibu wa vyombo vya habari kuhakikisha kuwa vinatekeleza wajibu wake
wa kuwaelimisha wananchi hao badala ya kuwapotosha.
Elimu kwa
wapiga kura ni muhimu sana kwa taifa lolote lile lenye kufuata misingi ya kidemokrasia.
Miongoni mwa faida kubwa ya elimu hiyo ni kuwafanya wapiga kura hao wake kwa
waume kuweza kuzitambua haki zao za msingi sambamba na mfumo mzima wa siasa
uliopo. Kuyatambua hayo kutawafanya wao wajue mtu gani wa kumchagua wakati wa
kupiga kura.
Pia inafaa
wananchi waelezwe ni kwa namna gani serikali iliyopo madarakani imetekeleza matakwa na maagizo yao waliyowatuma
kwa viongozi wao? Sambamba na hilo vyombo vya habari viangaze matendo yote
yaliyofanywa na viongozi wakati wa utawala wao (watchdog role). Kwa mfano
katika kipindi cha miaka kumi ya uongozi wa Jakaya Kikwete kuna mambo mengi
ambayo yamefanyika ikiwa ni kinyume na matakwa ya wananchi walio wengi. Hivyo
basi vyombo vya habari havina budi kulifafanua hilo.
Ni wajibu wa
vyombo vya habari kufanya kazi kwa ajili wa wananchi (Public service) badala ya
kufanya kazi ya chama kwa manufaa ya chama (Party service). Kufanya hivyo
itapelekea kuwa na vyombo vya habari bora na imara katika taifa letu.
Khelef
Nassor Al-riyamy
0772274011/
0718920331
Zanzibar.
0 comments :
Post a Comment